Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaanza mkutano wake wa 14 mjini Dodoma leo, huku kukiwa na homa ya matokeo ya mjadala wa Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2011/12.
Taarifa hiyo inatarajiwa kujadiliwa katika mkutano
huo sambamba na majibu ya awali ya Serikali kuhusu kasoro katika
matumizi ya fedha za umma zilizobainishwa na CAG, huku Kamati za Bunge
ya Hesabu za Serikali (PAC) na ile ya Hesabu za Serikali za Mitaa
(LAAC), zikitarajiwa kutoa taarifa ambazo zitakuwa mwongozo wa mjadala
bungeni.
Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah alisema jana
kuwa, kwa kawaida wabunge wanapaswa kujadili taarifa ya CAG kabla ya
mkutano wa Bunge la Bajeti ambalo hufanyika Aprili, ili kuwawezesha
kutoa maoni na maelekezo yanayopaswa kuzingatiwa katika mwaka wa fedha
unaofuata.
Kwa kuzingatia kalenda ya mikutano ya Bunge,
mkutano wa 14 ulipaswa kufanyika Februari 2014, lakini kama Spika Anne
Makinda alivyotangaza katika mkutano uliopita, unafanyika kuanzia leo
ili kutoa fursa kwa Bunge Maalumu la Katiba ambalo litakaa kati ya
Januari na Machi 2014.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,
Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema jana kuwa tayari Serikali
ilishawasilisha majibu ya awali kuhusu hoja za ukaguzi na kwamba baada
ya taarifa za LAAC na PAC kutakuwa na majibu ya nyongeza kwa hoja mpya
zitakazoibuliwa na kamati hizo.
“Serikali tayari ilishatoa majibu ya awali sasa
kwa sababu Kamati za PAC na LAAC zilikuwa zikikutana na watendaji wakuu
wa Serikali ambao taasisi au wizara zao zilionekana kuwa na kasoro
kwenye hesabu, tutawasikia watasema nini na hapo ndipo Serikali itatoa
tena ya nyongeza,” alisema Lukuvi.
Tangu Rais Jakaya Kikwete aliporidhia taarifa ya
CAG kuwasilishwa bungeni kisha kujadiliwa na wabunge, baadhi ya vigogo
wa Serikali wakiwamo mawaziri na watendaji wakuu ambao wizara na idara
wanazoziongoza zilibainika kuhusika na upotevu mkubwa wa fedha za umma
waling’olewa katika nafasi zao.
Katika mjadala wa mwaka jana, mawaziri sita na
naibu mawaziri wawili walitimuliwa kazi, yakiwa ni matokeo ya mjadala
mkali bungeni wa ripoti ya CAG ya 2010/2011. Mbali na vigogo hao, pia
fagio hilo liliwakumba wakurugenzi wakuu Shirika la Viwango Tanzania
(TBS) na yule wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).
Hali hiyo inatajwa kuwa moja ya sababu
zilizoisukuma Serikali kupeleka bungeni marekebisho katika Sheria ya
Ukaguzi wa Hesabu za Umma ya 2008, huku ikiongeza vifungu ambavyo
vilitafsiriwa kuwa vinapunguza nguvu ya Bunge katika kushughulikia
taarifa ya CAG.
Kwa maana hiyo, Bunge linajadili kwa mara ya
kwanza ripoti ya CAG tangu marekebisho ya sheria hiyo yanayozuia Bunge
kujadili ripoti ya CAG kabla Serikali haijajibu hoja za ukaguzi,
yapitishwe bungeni Februari mwaka huu.
Operesheni tokomeza
Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira
inatarajiwa kuwasilisha taarifa kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili
iliyoanza Oktoba 4 mwaka huu ikishirikisha Jeshi la Wananchi wa Tanzania
(JWTZ), Polisi, Usalama wa Taifa na Shirika la Hifadhi za Taifa
(Tanapa) kabla ya kusitishwa na Serikali Novemba Mosi.
No comments:
Post a Comment